Wednesday, 14 August 2013

Wadau washauri sheria itoe fursa sawa kwa wananchi


Wadau washauri sheria itoe

 fursa sawa kwa wananchi


 Serikali imeshauriwa kuongeza kifungu ambacho kitatoa fursa sawa kwa wananchi katika matumizi ya rasilimali maji.
“Tunaiomba Serikali kuongeza kifungu ambacho kitaweza kuwatetea wananchi wa kawaida pindi wanapotaka kutumia maji kwa ajili ya shughuli za kilimo,” alisema Pasiansi Mlowe kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).
Mlowe alitoa maoni hayo alipotoa maoni yake kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo,Maji na Umwagiliaji iliyokutana na wadau mbalimbali ili kujadili Muswada wa Sheria ya Umwagiliaji inayotarajiwa kuwasilishwa katika kikao kijacho cha Bunge.
Awali akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa kamati, Peter Msola alisema kuwa, lengo la mkutano huo ni kushirikisha wadau kutoa maoni yao kwenye vifungu ambavyo vina upungufu ili viweze kufanyiwa kazi kabla ya kwenda bungeni.
“Lengo letu ni kuhakikisha kuwa, muswada huu unakidhi matakwa ya wananchi, jambo ambalo limetufanya tushirikishe wadau mbalimbali ili waweze kujadili,” alisema Msola.
Alisema zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanategemea shughuli za kilimo, mpaka sasa kuna zaidi ya hekta 44 milioni nchi nzima, kati ya hizo ni asilimia 24 tu ndizo zinazotumika kwa ajili ya kilimo.
Alisema hekta 29.4 milioni zinafaa kwa matumizi ya kilimo cha umwagiliaji,huku hekta 450,000 ndizo zinazotumika kwa shughuli hiyo.
Alisema baada ya kufanya utafiti, wamebaini kuwa, hekta milioni 2.3 zinafaa kwa kiwango cha juu,huku hekta milioni 4.8 zinafaa kwa kiwango cha kati, kutokana na hali hiyo, Serikali imepanga kuboresha maeneo hayo ili yaweze kutumika katika shughuli hizo.
“Mkakati wetu ni kuhakikisha kuwa, sekta ya kilimo inakua kwa kasi,jambo ambalo linaweza kuwaondoa wananchi wengi katika hali ya umaskini,”aliongeza.
Alibainisha kuwa, kutokana na hali hiyo, Serikali imeboresha muswada huo ambao wanaamini unaweza kukidhi matakwa ya wananchi ambao wengi wao ni wakulima.
Hata hivyo, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chizza alisema kuwa, ikiwa sheria hiyo itafanyiwa marekebisho, wakulima wengi watakijikita kwenye kilimo cha umwagiliaji na si kusubiri kilimo cha msimu wa mvua.
“Hivi sasa wakulima wengi wanasubiri kilimo cha mvua za msimu, jambo ambalo limesababisha baadhi ya mikoa kuingia kwenye umaskini wa chakula, kutokana na kupitishwa kwa sheria hii kutasaidia kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kujiunga katika kilimo cha umwagiliaji,”alisema Chizza.


Aliongeza,licha Tanzania kulisha baadhi ya nchi zinazotuzunguka zikiwamo za Rwanda, Burundi, Kenya na Sudan Kusini, lakini bado kuna maeneo mengi ambayo hayatumiki.
Alisema kutokana na hali hiyo, wananchi wanapaswa kupewa elimu ili waweze kujua umuhimu wa kilimo hicho ambacho kitawakomboa katika shughuli zao.

No comments:

Post a Comment