WAKURUGENZI WA HALMASHAURI  WATUHUMIWA KWA UFISADI
 
 
WAKURUGENZI WA HALMASHAURI
 
 
 Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), imebaini mtandao wa 
ufisadi unaoshirikisha wakurugenzi 70 wa halmashauri mbalimbali hapa 
nchini ambao wanashirikiana na baadhi ya watendaji wa Ofisi ya Tawala za
 Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na Kitengo cha Hazina.
   
 Baadhi ya halmashauri hizo ni pamoja na Wilaya ya Monduli, Arusha, 
Mwanza, Mbeya na Ilala. Aidha Mwenyekiti wa kamati hiyo, Rajab Mohamed 
Mbarouk alisema keshokutwa atataja majina ya wakurugenzi hao ili 
wananchi waweze kuwafahamu.
 Mbarouk 
alisema kuwa Tanzania Bara ina halmashauri 134, kwa hiyo ina maana zaidi
 ya nusu ya wakurugenzi wanajihusisha na mambo hayo.
 
 “Baadhi ya
 wakurugenzi hao walihamishwa kwenye vituo vyao vya kazi kutokana na 
kashfa ya matumizi mabaya ya fedha za Serikali, lakini bado 
wanajihusisha na mambo haya,” alisema Mbarouk.
 
 Alisema kutokana
 na hali hiyo, kamati hiyo imepanga kukutana kesho na Waziri Mkuu, 
Mizengo Pinda na Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia ili kuzungumzia suala 
hilo.
 
 Aliongeza wakurugenzi hao wamekuwa wakishirikiana na 
wahasibu wao katika kutumia vibaya fedha za Serikali zinazotolewa kwa 
ajili ya kuendeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika halmashauri 
zao.
 
 Akitolea mfano wa Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Wilson 
Kabwe ambapo halmashauri yake imefanya vibaya katika ripoti ya Mdhibiti 
na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), lakini hajachukuliwa hatua 
na badala yake amekuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam.
 
 
Alisema mbali na halmashauri hiyo, aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa 
Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Rhoda Nsemwa ambaye alisimamishwa 
kazi kutokana na tuhuma za ufisadi, lakini bado anaendelea kupata 
mshahara na stahiki zake kama mtumishi aliye kazini.

 
 
 
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment