Nanenane ni ya wakulima,
 siyo Serikali
|  | 
| chui wa Tanzania | 
|  | 
| Tembo wa Tanzania | 
Waasisi wa programu ya kuifanya siku hiyo iwe 
rasmi kwa wakulima walitaka wakulima watumie siku hiyo kama fursa ya 
kuonyesha mazao yao, kubadilishana mawazo miongoni mwao kuhusu kilimo na
 kutafuta namna ya kukabiliana na changamoto zinazowakabili kwa lengo la
 kuongeza tija na uzalishaji.
Pia maadhimisho hayo yalilenga kuwasaidia wakulima
 kufanya mashauriano kuhusu namna ya kupata masoko ya kuwapatia bei 
nzuri kwa mazao yao.
Masuala ya pembejeo za kilimo na mbinu za 
kufanikisha kilimo cha kisasa yalipewa kipaumbele siku hiyo, kwani 
wakati huo wataalamu wa kilimo na ‘mabwanashamba’ walikuwa sambamba na 
wakulima na viongozi wa vyama vya ushirika ili kuwapa ushauri katika 
maeneo husika.
Wakati huo wakulima walikuwa wakijiona kama wadau 
muhimu katika sekta ya kilimo na vyama vya ushirika vilikuwa 
vikiwajibika kwao kikamilifu, tofauti kabisa na hali ilivyo hivi sasa.
Inasikitisha kuona kwamba hivi sasa sio tu 
maadhimisho hayo hayawahusishi tena wakulima katika kiwango tulichokijua
 wakati ule, bali pia yametekwa na taasisi za Serikali, wanasiasa na 
wakala wa maendeleo wasiohusika na kilimo hata kidogo.
Kila wizara, mashirika ya umma na idara za 
Serikali zimejenga mabanda ya maonyesho kwa gharama kubwa ili kutumia 
siku hiyo kutangaza bidhaa na shughuli zake, nyingi zikiwa hazina 
uhusiano wowote na masuala ya kilimo, hivyo kuifanya Siku ya Wakulima 
kupoteza maana ya kuanzishwa kwake.
Shamrashamra za wakulima tulizokuwa tukizishuhudia
 siku hiyo zimepotea kutokana na viongozi wa Serikali na wanasiasa 
kuteka siku hiyo kwa sababu za kimasilahi.
Mkanganyiko kuhusu siku ya kilele cha maonyesho ya
 Siku ya Wakulima umetokana na kuwapo mkono wa Serikali katika maonyesho
 hayo ya wakulima.
Badala ya kukiachia Chama cha Wakulima Tanzania 
(Taso), kitekeleze jukumu lake la kuratibu maonyesho hayo, ikiwa ni 
pamoja na kuamua siku ya kilele cha maonyesho hayo kutokana na uwezekano
 wa kuingiliana na Sikukuu ya Iddi el Fitri, Serikali imepenyeza mkono 
wake na kuamua kwamba jana ndio iwe siku ya kilele cha maonyesho hayo. 
Matokeo yake ni mkanganyiko, kwani kanda nyingine, ikiwamo Mbeya 
zimeamua kilele hicho kiwe leo.
Katika siku za hivi karibuni zimejitokeza sauti 
kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini zikitaka ifanyike tathmini juu ya 
ubora wa maonyesho hayo katika miaka 10 iliyopita ili kuona kama 
yamekuwa yakifanyika kulingana na malengo ya kuanzishwa kwake.
Moja ya sauti hizo ni ile ya Mkuu wa Mkoa wa 
Manyara, Erasto Mbwilo ambaye wakati akifungua maonyesho hayo Kanda ya 
Arusha, alisema tathmini hiyo itaonyesha kama yana faida au hasara na 
kuongeza kwamba huenda yakatumia gharama kubwa pasipo kuwasaidia 
wananchi.
Tunaungana na mkuu huyo wa Mkoa na wengine wengi ambao wameuliza
 maswali kuhusu ubora na umuhimu wa maonyesho hayo katika muktadha wa 
gharama kubwa zinazotumika kuyaendesha.
Kama tulivyosema hapo juu, kimsingi wakulima ndio 
walikuwa walengwa wakubwa wa maonyesho hayo, lakini sote tumeshuhudia 
Serikali na wanasiasa wakiyapa sura ya kibiashara, huku wakulima 
wakipigwa changa la macho.

No comments:
Post a Comment